Saturday 2 April 2016

Paul Makonda aahidi neema kwa waendesha bodaboda

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amekutana na waendesha pikipiki za kubeba abiria maarufu kama Bodaboda mkoani Dar na kuwapa ahadi nono za kuwainua kimaisha kupitia biashara hiyo.

Pamoja na mambo mengine, Makonda ameahidi kuwapa pikipiki bodaboda hao kwa marejesho ya shilingi 25,000 kwa wiki (sawa na shilingi 3,500) kwa siku na baadae kuwaachia wazimiliki wao.

Katika hatua nyingine, Makonda ameahidi kuwatengenezea mpango mzuri  utakaowawezesha bodaboda hao kuingia katikati ya Jiji, tofauti na ilivyo sasa.

Mwakilishi wa Bodaboda, Daud Laurian alitaja changamoto zinazowakabili kuwa ni zuio la kuingia mjini (CBD) la Machi 3,2014.
“Tumekutana na changamoto nyingi, kwa mfano kutozwa faini kuanzia Sh50,000 hadi zaidi ya 400,000, kukamatwa kinyama na kufukuzwa na magari,” alisema.

Ahadi ya Makonda kuwaruhusu Bodaboda kuingia Jijini ni ukamilifu wa ahadi ya Rais John Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka jana.

Juzi, Meya mpya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita (Chadema) pia aliahidi kuhakikisha Bodaboda wanaweza kuingia mjini kwa utaratibu maalum.

No comments:

Post a Comment